NA MWANDISHI WETU,MWANZA
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa watoaji wa huduma za kifedha nchini kutazama upya masharti ya mikopo, ikiwemo dhamana ya mali zisizohamishika kwa kuwa ni kikwazo kwa wajasiriamali.
Dkt.Mpango ameyasema hayo leo Novemba24,2022 wakati akifungua Maadhimisho ya Pili ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yanayofanyika Jijini Mwanza.
Aidha amesema riba ya mikopo ya wastani wa asilimia 16 bado ni mzigo kwa Watanzania walio wengi hivyo amesisitiza kila benki kupitia umoja wao (TBA) kuchambua mizizi ya changamoto hiyo na kupunguza zaidi riba kwa wakopaji.
Halikadhalika,Makamu wa Rais ametoa wito kwa watoaji wa huduma za kifedha nchini kupunguza gharama za kutuma na kupokea pesa kimataifa kwa kuwa zimekua zikisababisha wageni pamoja na diaspora kutumia njia zisizo rasmi wanapowatumia pesa jamaa zao hapa nchini.
Ameongeza kwamba kwa upande wa credit cards, tozo za benki na mawakala wao zimekuwa mzigo na hivyo kukwamisha watalii kununua vitu kwa wingi na kuikosesha mapato Serikali na watoa huduma mbalimbali.
Pia ameutaka Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA) kusaidia kuhamasisha wanachama wao kutanua wigo wa huduma za kifedha katika maeneo ya vijijini pamoja na mkopeshe zaidi na kukuza akiba ili kupunguza utamaduni wa wananchi kutunza pesa katika mfumo usio rasmi.
Makamu wa Rais ametoa wito kwa Benki Kuu ya Tanzania kutoa elimu na mwongozo kuhusu fursa na hatari zinazoambatana na maendeleo ya wimbi la fedha za kidigitali (Central Bank Digital Currency, cryptocurrencies, bitcoins n.k.)ambayo yanaigusa jamii hususan vijana na baadhi ya wastaafu wenye kiu ya kuwekeza huko.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Hamad Chande amesema kupitia maboresho yaliofanyika katika Sekta ya Fedha nchini jumla ya Sh. Trilioni 3.99 imekopeshwa kwa sekta binafsi ikiwa ni ukuaji wa asilimia 19.4, kuchangia ukuaji wa pato la taifa kwa asilimia 4.9 kwa mwaka 2021 pamoja na kuongezeka kwa matumizi ya huduma za fedha kwa njia ya simu kufikia akaunti milioni 33.14.
Chande amesema sekta ya fedha inakabiliwa na changamoto mbalimbali nchini ikiwemo wananchi kutumia huduma za fedha zisizo rasmi kama vile biashara haramu ya upatu , biashara zisizo rasmi kwa njia ya mtandao pamoja na idadi kubwa ya wananchi kutokuwa na uelewa wan kutosha kuhusu teknolojia ya masuala ya fedha.




Discussion about this post