NA MWANDISHI WETU
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa Viongozi wa dini zote, wakiwemo wa Kimila na Wazee hapa nchini kusaidia kulea watoto na vijana kimaadili ili kuweka mustakabali wa taifa na watu wake kwenye mikono salama.
Makamu wa Rais ameyasema hayo leo Novemba 28,2022 jijini Dar es Salaam wakati alipomwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika Ufunguzi wa Kongamano la Kitaifa la Maadili la Viongozi wa Dini wa Kamati za Amani na Jumuiya ya Maridhiano Tanzania.
Amesema vijana wakifundishwa mila na desturi sahihi na kushika mafundisho ya dini, na wakawa na hofu ya Mwenyezi Mungu, maovu mengi yatapungua hapa nchini.
Dkt.Mpango amefafanua kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango wa Dini zote katika kujenga maadili mema ndani ya jamii ya watanzania.
Aidha amewasihi viongozi wa dini kuendelea kuliombea Taifa, viongozi na watumishi wa Serikali bila kuchoka ili kutekeleza vema mipango ya maendeleo ya nchi na watu wake.
Aidha amekemea vikali ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto wa kike na kiume hapa nchini na kuviagiza vyombo vya dola kuongeza nguvu katika kupambana na ukatili huo.
Amewataka pia walezi na wazazi kuweka mifumo imara ya ulinzi kwa watoto katika ngazi ya familia, mtaa, mashuleni, madrasa, vyuoni na sehemu nyingine ili kulinda haki na ustawi wa watoto na kuwaepusha na vitendo vya ukatili vinavyofanyika dhidi yao.
Dkt.Mpango amewakumbusha viongozi wa dini hapa nchini kukemea vitendo vya Rushwa na Ufisadi kupitia nyumba za ibada pamoja na kuwaelimisha wananchi madhara ya kutoa na kupokea rushwa na kushiriki kuhujumu mali za umma.
“Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya utoaji huduma ili kudhibiti vitendo vya rushwa na ufisadi pamoja na kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu yeyote atakayejihusisha na vitendo hivi bila kujali cheo au nafasi yake katika jamii”amebainisha Dkt Mpango
Dkt.Mpango amewasihi wazazi na walezi kwa pamoja kushiriki katika mapambano ya kudhibiti matumizi ya dawa za kulevya kwa kutoa elimu kwa jamii pamoja na kutoa taarifa na kuwafichua wote wanajishughulisha na biashara hiyo haramu inayoathiri afya za vijana hapa nchini.
Katika hatua nyingine Makamu wa Rais amewaasa Viongozi wa dini kujiepusha na migogoro ndani ya Taasisi zao ambayo imekuwa ikisababishwa na uchu wa madaraka, ubinafsi, uchu wa fedha, matumizi mabaya ya mali za taasisi za dini na ukiukwaji wa katiba za taasisi za dini.
Amewahimiza viongozi hao wa dini kusuluhisha mapema migogoro ndani ya taasisi zao inapojitokeza kwa kuzingatia sheria, miongozo na taratibu zinazokubalika ili wawe mfano mzuri wa maadili kwa jamii ya watanzania.
Kwa Upande Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhandisi Hamad Masauni amesema Wizara hiyo imeanzisha mfumo wa usajili na usimamizi wa jumuiya hpa nchini unaolenga kusaidia changamoto mbalimbali ambazo zilikua zikilalamikiwa ikiwemo ucheleweshaji wa usajili Jumuiya pamoja na kutopata taarifa mbalimbali.
Mwenyekiti wa Kamati za Amani na Jumuiya ya Maridhiano Tanzania Sheikh Alhad Mussa Salum amesema wataendelea kushirikiana na serikali katika kukabiliana na mmomonyoko wa maadili uliopo hapa nchini.
Awali akisoma Risala Katibu Mkuu, Jumuiya ya Maridhiano Tanzania Mchungaji Dkt. Israel Maasa amesema Jumuiya hiyo imeweza kufanya mambo mbalimbali ikiwemo kumaliza migogoro mbalimbali kati ya wakulima na wafugaji, kupambana na mila potofu pamoja na kupambana na ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na Watoto.




Discussion about this post