NA MWANDISHI WETU,SHINYANGA
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Philip Mpango amekemea tabia ya wizi wa maji inayofanywa na baadhi ya watu nchini wakiwemo wawekezaji wakubwa na kuzitaka mamlaka husika kuacha kutoza faini ndogo kwa wanaokutwa na hatia za wizi wa maji.
Aidha amevitaka vyombo vyote husika kufuatilia na kuwachukulia hatua wezi wote pamoja na wale wanaochepusha maji kutoka kwenye mito bila vibali halali na wengine kuharibu vyanzo vya maji.
Makamu wa Rais amesema hayo wakati akiweka Jiwe la Msingi Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria Tinde mkoani Sinyanga Januari 19,2023 ambao utakaohudumia Tinde na Shelui unaogharimu Sh.Bilioni 24.4.
Amesema ni muhimu Mamlaka za Maji pamoja na wadau wengine wa sekta hiyo kuongeza weledi katika usimamizi wa rasilimali za maji kwa kujenga miundombinu mingi zaidi ya kutunza maji na kuvuna maji ya mvua ili kukabiliana na changamoto za maji ambazo hujitokeza.
Aidha Dkt. Mpango amesema dhamira ya Serikali ni kuona mradi huo unatoa maji na kuwa endelevu kwa wananchi kama ilivyokusudiwa na pia juhudi za kupeleka maji katika maeneo yaliyopo karibu na mradi huo zinaendelea ikiwa ni pamoja na kuhakikisha maeneo yote yanapata majisafi na salama na yanatosheleza mahitaji.
“Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imeamua kutoa kipaumbele cha juu kugharamia miradi ya maji ili itoe huduma endelevu ya majisafi na salama pamoja na elimu ya usafi wa mazingira kwa wananchi wote.
“Sekta hiyo ni miongoni mwa Sekta za kipaumbele katika Mkakati wa kukuza Uchumi wa Viwanda na kupambana na umaskini nchini na kuboresha huduma ya maji kutapunguza muda wa kutafuta na kuchota maji ili kuwawezesha Wananchi kufanya kazi nyingine za maendeleo,kuongezeka kwa muda wa Wanafunzi kuhudhuria masomo, kuimarisha afya za Wananchi na kuepusha magonjwa yanayotokana na matumizi ya maji yasiyo safi na salama.
“Tunataka muongeza ufanisi katika matumizi ya maji, hususan kwenye kilimo pamoja na kuwaagiza kutunza vyanzo vya maji ikiwemo chanzo cha Ziwa Victoria kilichopo Ihelele Wilayani Misungwi, ambacho ni tegemeo kwa upatikanaji wa huduma za maji katika Miji ya Wilaya za Misungwi, Kahama, Shinyanga, Tabora, Kahama, Nzega, Igunga, Shelui na Tinde”amesema Dkt.Mpango
Kwa upande wake Waziri wa Maji Jumaa Aweso amesema Wizara hiyo inatekeleza miradi ya maji ya kimkakati katika mkoa wa Shinyanga inayogharimu shilingi bilioni 35 itakayosaidia kwa kiasi kikubwa wananchi wa mkoa huo kuondokana na changamoto za upatikanaji wa maji safi na salama.
Aweso amebainisha kuwa pamoja na wananchi wa Kata ya Tinde kunufaika na mradi huo,lakini pia vijiji 22 vya jirani vitaweza kufikiwa na mradi utakaowasaidia wananchi kupata maji safi na salama.
“Wizara itaendelea kufuatilia na kusimamia kwa makini utekelezwaji wa miradi ya maji ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kutoka huduma kwa wananchi katika kufikia adhma ya kufikisha maji kwa asilimia 95 maeneo ya mijini na asilimia 85 maeneo ya vijijini ifikapo mwaka 2025”amefafanua Aweso




Discussion about this post