NA MWANDISHI WETU,MOROGORO
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Daniel Chongolo amesema Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro ni maarufu kwa migogoro ya ardhi na kuwataka viongozi wa ngazi zote kuhakikisha wanatatua hali hiyo kwenye maeneo wanayoyasimamia kiutawala.
Amesema lengo la CCM na Serikali kwa ujumla ni kuona changamoto za wananchi zinapatiwa majawabu hivyo hawawezi kuwa na viongozi wanaosababisha mgogoro kila siku hivyo lazima wafanye maamuzi na wasimamie wanayoyaamua
Akizungumza na Wananchi pamoja na Wanachama wa chama hicho Januari 29,2023 katika Kata ya Dakawa wilayani Mvomero Mkoa wa Morogoro, Chongolo amesema Serikali inayoongozwa na CCM inaendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi kwenye maeneo husika huku akieleza changamoto kubwa kwenye wilaya ya Mvomero ni migogoro ya ardhi.
“Mimi na wenzangu tumekuja Mvomero kwa ajili ya kuzungumza na wananchi, kusalimiana na kusikiliza changamoto zao,nimepewa changamoto ya migogoro ya ardhi kati ya Kijiji na Kijiji, Kata na Kata na maeneo ya kiutawala na changamoto hizi mara nyingi zinasababishwa na viongozi ambao wanaongeza maeneo ili kupata kura na baadae anaacha kero kwa wananchi.
“Sisi viongozi ndio wenye jukumu la kutatua changamoto ,Sheria ya nchi iko wazi kwa sababu hakuna kijiji kisicho na mpaka kwani maeneo yote yameanishwa , ukiona kuna shida ya kijiji na kijiji uje viongozi wenyewe ndio wanashida,nimeona nianze na hilo kwasababu Mvomero ni maarufu kwa migogoro ya ardhi.”Amesema Chongolo
Chongolo ameongeza kuwa ni lazima viongozi waamue kumaliza changamoto ambazo hazina haja ya kulelewa kwa muda mrefu ikiwemo changamoto ya mipaka ya kiutawala iwe ngazi ya Kijiji Kata,Wilaya na Mkoa , na linawezekana kama viongozi watakubali.
Aidha amebainisha kuwa kumekuwepo na utaratibu wa kuweka mipango ya matumizi bora ya ardhi kwa kutenga maeneo kwa ajili ya makazi, kilimo na ufugaji lakini bado kumekuwa kukiibuka changamoto na kueleza kuwa wakulima wakipewa eneo wanalima hao hao lakini mfugaji akipewa eneo la mifugo anaalika na wenzake baada ya miezi sita anahangaika kutafuta malisho.
“Sababu mkulima hajaalika wengine kuja kulima kwenye shamba lake lakini mfugaji amealika na wenzake, hii mialiko kuna wanaosaidia kuifanikisha , ng’ombe haruki kama njiwa , lazima atembee anakopita kuna viongozi na wanaona, hatuwezi viongozi tunakuja kila siku tunaambiwa mgogoro wa wakulima , mgogoro wa wafugaji”amesema Chongolo.




Discussion about this post