NA MWANDISHI WETU
WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kujikita katika kuandika habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu ili kuwasaidia wananchi kupata taarifa za kitafiti kwa lugha walioizoea.
Wananchi wengi wamekuwa wakikosa fursa mbalimbali za maendelo na kutatua changamoto zao kutoka na tafiti nyingi za Sayansi na Teknolojia kushindwa kuwafikia kutokana na kile kinachoelezwa kuwa lugha ngumu inayotumika hivyo wananchi wengi kukosa fursa ya kujua umuhimu na matokea ya tafiti hizo katika maisha yao ya kila siku.
Hata hivyo Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) chini ya Mkurugenzi wake Dkt.Amos Nungu imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali ili kuhakikisha kuwa taarifa za kisayansi na teknolojia zinawafikia wananchi wa hali ya chini kupitia vyombo vya habari.
Akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakati wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kati ya waandishi wa habari na watafiti yaliyoandaliwa na COSTECH,Afisa Mratibu Utafiti Mwandamizi kutoka Tume hiyo Method Retachura amesema baadhi ya majukumu ya Tume hiyo ni pamoja na kukusanya,kuchakata,kuhifadhi na kusambaza taarifa za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu
Amebainisha kuwa jukumu lingeni ni pamoja na Kuishauri Serikali kuhusu masuala ya sayansi, teknolojia na ubunifu yakiwemo vipaumbele vya utafiti, mgawo wa matumizi ya fedha za utafiti kufuatana na vipaumbele vilivyokubaliwa, ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika utafiti, mafunzo na ajira za watafiti, pamoja na Sera ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia.
Akizungumzia mbinu za uandishi wa habari za kitafiti,Retachura amesema ni muhimu kujua utafiti umegundua kitu gani kipya (findings) ambacho kinatakiwa kuwasilishwa kwa umma unaoweza kuboresha kipato, kuondoa maradhi, kuboresha teknolojia au kuongeza mavuno ya kilimo na mengine.
Aidha amefafanua kuwa mbali na hilo lakini pia mwandishi ni muhimu kufahamu athari za utafiti (research impact) ili kusaidia jamii kujua mambo muhimu yanaendelea kwa manufaa ya Taifa zima.
Akizungumzia kuhusu wajibu Mwandishi wa Habari,Retachura ameeleza kuwa baada ya kupata taarifa za utafiti kupitia njia sahihi ni wajibu wa mwanahabari kuripoti kwa mujibu wa sera ya habari ya taasisi yake (Editorial Policy).
Aisha Retachura amesema taarifa za msingi zifikishwe bila ya kupotoshwa au kutiwa chumvi(kuongezea maneno mengine) kwa madhumuni ya kutia hofu umma.
“Taarifa za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu zinaungwa mkono, au kutofautishwa na taarifa nyingine, kwa kutumia lugha ya takwimu na ukweli.
“Ninaamini mfumo huu utasaidia mno kufikisha taarifa za utafiti wa kisayansi kwa umma.
“Aidha, malalamiko ya kwamba waandishi hawafahamu taarifa zilizomo katika tafiti yatapungua kwa kiwango kikubwa”amesema Retachura
Kwa upande wake Mratibu wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kutoka COSTECH Deusideth Leoanaed amesema hayo ni mafunzo ya tisa kufanyika tangu mwaka 2015 ya kuwakutanisha Waandishi wa Habari,Watafiti na Wabunifu.
“Lengo ni kuwaleta pamoja na kubadilishana uzoefu ili tafiti nyingi ziweze kuandikwa kwa lugha rahisi,kupata ongezeko la uhawilishaji wa teknolojia kati ya Watafiti na Jamii na kuwajengea uwezo waandishi wa habari ili waweze kuandika taarifa za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kama ilivyo katika maeneo mengine ikiwemo siasa na michezo”amesema Leonaed.
Waandishi mbalimbali wa habari kutoka katika magazeti,luninga,redio na blog wamefanikiwa kupata mafunzo juu ya kuandika Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu ili kusaidia katika kufikisha taarifa sahihi kwa wananchi kwa lengo la kutatua changamoto zinazowakabili.




Discussion about this post