Exuperius Kachenje
RAIS Dkt.Samia Suluhu Hassan amewataka Wahariri wa Vyombo vya Habari nchini kufanya kazi kwa kuzingatia maadili ya taaluma ya habari na haoni sababu ya kuminya uhuru wa habari.
Hata hivyo amewataka pia kufanya kazi zao bila upendeleo wala kumuonea mtu ikiwemo kutoogopa wanapotekeleza majukumu yao ya kikazi.
Rais Dk. Samia ametoa rai hiyo Machi 29,2023 mjini Morogoro katika salam zake kwa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF’), linalofanya mkutano wake wa 12 wa mwaka wa kitaaluma.
Akitoa salam hizo za Rais mbele ya wahariri wa vyombo vya habari, Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesema Rais amemtuma awaambie kuwa wafanye kazi bila woga,kitaaluma na pasipo upendeleo wala kumuonea mtu.
Nape aliyekuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa mkutano huo alifafanua kuwa Rais Dkt. Samia aliwahi kumwambia wakati wa mchakato wa kupitia Sheria ya Habari kwamba wahakikishe hawaingilii haki ya watu kujieleza.
“Rais kanituma, waambie wafanye kazi bila woga, kitaaluma, bila upendeleo wala kumuonea mtu,haya ni maneno ya Rais mwenyewe.”amesema Nape
Amesema Rais Dkt.Samia ni muumini wa haki ya kujieleza na kutoa maoni hivyo haoni sababu ya kuminya uhuru wa habari.
Nape alivitaka vyombo ya habari kuandika habari za kiuchunguzi zenye lengo la kulisaidia taifa pamoja na wahariri kusaidia kurithisha weledi waandishi vijana hasa kwenye mitandao ya kijamii akieleza kuwa eneo hilo lina shida kidogo ya weledi.
Aidha ameongeza kuwa ingawa vyombo vya habari vinayumba kiuchumi kwa sababu mbalimbali ikiwamo kutolipwa madeni yanayofikia Sh.Bilioni 18, kuna madai ya wahariri na waandishi kwa vyombo hivyo kuwa hawalipwi mishahara.
“Tutavibana vyombo vishughulikiea maslahi ya wahariri na waandishi,” amesema Nape
Akizungumzia kuhusu alivyoshughulikia uvamizi wa kituo cha luninga na redio cha Clouds Media uliofanywa na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda,Nape amebainisha kuwa wakati anajiandaa kuwasilisha ripoti hiyo, alizuiwa kufanya hivyo na mwajiri wake na kuagizwa ikiwa ataitoa atapoteza ajira.
“Niliambiwa nisiendelee na uchunguzi au nitapoteza ajira, nikachagua heshima, lakini leo nipo hapa,” amesema Nape.
Mwezi Machi 2017 Makonda akiwa na askari polisi waliokuwa na bunduki aliingia katika ofisi za studio za redio na Televisheni ya Clouds majira ya saa 4:46 usiku huku baadhi ya vipindi vikiwa vinaendelea kwa kuendeshwa na watangazaji wa zamu wa kipindi maarufu cha Shilawadu kilichokuwa chini ya Mtangazaji ‘Soudy Brown’.
Naye Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile alimshukuru Rais Dk.Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Habari na watendaji wake kwa ushirikiano na vyombo vya habari unaowezesha ukuaji wa vyombo hivyo.
“Idadi ya kesi kwa vyombo vya habari imepungua, mwaka sasa hakuna shitaka jipya,hii ni ishara njema ya ukuaji vyombo vya habari, hata kimataifa tulikuwa wa 124 mwaka 2021 lakini mwaka 2022 tumekuwa wa 12,”amesema Balile.
Hata hivyo, Balile aongeza kuwa pamoja na matumaini hayo mapya, hali ya uchumi wa vyombo vya habari si nzurii na kuikumbusha Serikali deni la takribani Sh.Bilioni 20 ambazo vyombo vya habari vinadai kwa wadau mbalimbali ikiwemo.




Discussion about this post