TOKYO,JAPAN
SERIKALI ya Japan imeanza kuonja athari za uzazi wa mpango baada ya kushuhudia kushuka kwa kiwango cha watu kuzaliana.
Kushuka huko kwa kiwango cha kuzaliana kimeishtua Serikali ya nchi hiyo na kuahidi kuanza kutoa ruzuku kwa watoto hadi watakapofika elimu ya sekondari ikiwa ni jaribio la kukabiliana na hali inayoendelea ya kushuka kwa kiwango cha kuzaliana nchini humo
Nchi hiyo iliyo jirani na China,Korea Kusini na Kaskazini imeshuhudia mwaka 2022 kuzaliwa watoto wachache chini ya 800,000 ikiwa ni rekodi ya chini zaidi.
Hata hivyo Serikali ya nchi hiyo imepanga kutoa malipo kwa watoto watakaozaliwa hadi watakapohitimu sekondari ya juu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Aprili Mosi,2023 na Shirika la Habari la Japan (NHK) imeeleza kuwa Japani inapendekeza uboreshaji wa huduma za matunzo ya watoto na ongezeko la ruzuku za serikali ili kukabiliana na hali hiyo..
Mapendekezo hayo ni sehemu ya ahadi ya Waziri Mkuu wa nchi hiyo Kishida Fumio kuchukua kile alichokiita “hatua za kipekee” kushughulikia tatizo hilo.
Idadi ya watoto wanaozaliwa inapungua kwa kasi kuliko ilivyotarajiwa ambapo Serikali ya nchi hiyo ilitoa rasimu ya kwanza ya mapendekezo yake Machi 30,2023,lengo likiwa ni kuyatekeleza ndani ya kipindi cha miaka mitatu kuanzia Aprili 2024.
Mapendekezo hayo yanajumuisha kuondoa ukomo wa kipato katika ruzuku za serikali kwa wazazi na Serikali inapanga kuja na muhtasari wa bajeti kwa ajili ya mapendekezo hayo kufikia mwezi Juni mwaka 2023.




Discussion about this post