NA MWANDISHI WETU,TANGA
SHIRIKISHO la Vyama vya Watu Wenye Walemavu Tanzania (SHIVYAWATA) limeshukuru kuwepo kwa mfumo wa kusaidia watu wenye ulemavu wa miguu kuendesha gari kwa kuwa hali hiyo inaonesha jinsi Serikali na watanzania wengine wanavyowakumbuka wenye hali hiyo.
Hayo yameelezwa Aprili 11,2023 na Mwenyekiti wa SHIVYAWATA Ernest Kimaya wakati akizungumza na tovuti hii ya Bajeti juu ya mfumo huo ambao umebuniwa na mtanzania Joseph Taifa unaowafanya watu wenye ulemavu wa miguu kuendesha gari kama walivyo wengine.
Amesema wamefurahi kusikia watanzania wengine wanawakumbuka na kuwajali watu wenye ulemavu hadi kufikia hatua ya kubuni kitu hicho cha kuwafanya nao kuendesha vyombo vya moto vyenye vifaa vinavyoendana na mazingira yao.
“Tunaishukuru sana Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwa kuendeleza ubunifu huo ili watu wenye ulemavu wa miguu nao waweze kutumia magari,tunashukuru sana na sisi tutasambaza nchi nzima ili ufahamike”amesema Kimaya
Haya hivyo Kimaya amebainisha kuwa wanajipanga ili kutembelea karakana ya mbunifu huyo kujionea anavyotengeneza na kuona jinsi gani ya kuuendeleza ili kuwanufaisha watu wenye ulemavu nchi nzima.

Kwa upande wake Mtafiti na Mbunifu huyo Joseph Taifa amesema amefurahi kusikia kitu alichokibuni kinaweza kuwasaidia watu wengi wenye ulemavu wa miguu ambao walikata tamaa ya kuendesha gari kutokana na hali waliyokuwa nayo na alitumia muda mwingi kuwafikiria baada ya kuhitimu masomo yake chuoni.
“Tunawasubiri sana SHIVYAWATA ili tuwaonesha mfumo huu ambao ili mtu mwenye ulemavu aweze kuendesha gari lazima pia asome kwanza chuo ambacho tunaendelea na maandalizi ya mwisho ili kukamilisha taratibu za kiserikali ambapo hadi sasa tumeshafunga magari matatu.
“Lazima kila dereva anayetumia mfumo huu asome chuo kwa kuwa anaweza kusababisha ajali kwa kushindwa kumudu kulisimamisha ama kuondoka kutokana na vifaa vyake vingi kutumia mikono pekee na sio miguu”amesema Taifa
Hata hivypo Taifa ameongeza kuwa mfumo huo hauruhusu gari kuharibika na kwamba unaweza kufungwa ama kuondolewa katika gari bila tatizo..




Discussion about this post