NA MWANDISHI WETU,DODOMA
HALMASHAURI ya Wilaya ya Kaliua mkoani Tabora imejipanga kuanzisha mradi wa hifadhi ya misitu kwa ajili ya biashara ya kaboni.
Hayo yamebainika Juni 06, 2023 jijini Dodoma wakati Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Selemani Jafo alipofanya kikao na Mkuu wa Wilaya ya Kaliua Dkt. Rashid Chuachua pamoja na ujumbe wake waliomtembelea kwa ili kuwasilisha taarifa ya kusudio la kuanzisha mradi wa hifadhi za misitu kwa ajili ya biashara ya Kaboni.
Akizungumza mara baada ya mkutano huo,Jafo amesema Serikali inaendelea kufungua milango kwa wawekezaji wa Biashara ili kuhifadhi mazingira.
Amesema Ofisi ya Makamu wa Rais ipo tayari kuendelea kutoa elimu kwa umma ili kuwapa uelewa wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini zikiwemo halmashauri kuhusu faida za kupanda miti na kuhifadhi misitu.
“Kutokana na Mikataba ya Kimataifa ya Mabadilkiko ya Tabianchi, sisi kama nchi tumejipanga vizuri kuhakikisha wananchi wanafaidika na biashara hii na ndio maana tumeandaa kanuni na mwongozo,” amesema Jafo.
Aidha ameupongeza uongozi wa wilaya hiyo kwa kuhifadhi misitu na nia yao ya kuwekeza katika biashara ya Kaboni akisema kuwa mbali ya kuhifadhi mazingira lakini pia itakuwa chanzo cha mapato ya halmashauri.
Kwa upande wake Dkt. Chuachua amesema kusudio la kuanzisha mradi wa hifadhi ya misitu kwa ajili ya hewa ya ukaa ni kupata fursa ya biashara hiyo ambayo faida yake itasaidia kuboresha huduma kwa wananchi wake.
Amesema wilaya ina fursa kubwa ya kuwekeza katika biashara hiyo kwa kuzingatia kuwa ina kilomita za mraba 12,084.5 sawa na asilimia 86 ya eneo lote la wilaya hiyo.
“Mradi huu ni muhimu kwani utasaidia kuongeza wigo wa mapato ya halmashauri ambayo kwa asilimia 80 yamekuwa yakitokana na mazao ya kilimo lakini pia utasaidia katika kutunza mazingira ya ardhi oevu ambayo ndio chanzo cha maji katika Mto Malagarasi na Ziwa Tanganyika”amesema Dkt.Chuachua
Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Andrew Komba amebainisha kuwa Biashara ya Kaboni Kimataifa inasimamiwa na Umoja wa Mataifa kwa lengo kuwezesha nchi wanachama kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Dkt. Komba ameongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi yanasababisha ongezeko la joto duniani na vipndi vya baridi na mvua kupungua hali inayochangia ukame hivyo uwepo wa misitu mingi itasaidia katika kunyonya gesijoto inayochangiwa na shughuli za kibinadamu zikiwemo moshi unaotokana na magari na viwanda.




Discussion about this post