NA MWANDISHI WETU
BAADHI ya watafiti na wabunifu wa vitu mbalimbali vya sayansi na kiteknolojia wameishukuru Serikali kwa kuwapatia kiasi cha Sh. Bilioni 1.191 zitakazosaidia kuendeleza bunifu zao.
Mbali na kiasi hicho lakini pia Serikali imetoa kiasi cha Sh.Bilioni 2.5, kwa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) ili zitumike kuwakopesha wabunifu.
Kutolewa kwa fedha hizo na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan zitasaidia katika kuongeza soko la ajira ambapo wabunifu hao watazitumia kuajiri vijana wenzao katika kuendeleza bunifu zao.
Akizungumza na Bajeti Communication jijini Dar es Salaam Juni 24,2023,Mbunifu na Mtafiti wa Kaboni inayotokana na vifuu vya nazi Tiberius Mario amesema anaishukuru sana Serikali kutoa kiasi hicho cha fedha ambapo kitagawanywa kwa wabunifu 49.
Amesema yeye alipokea hundi ya kiasi cha Sh.Bilioni 1.10 kwa niaba ya wenzake 48 wakati wa Mkutano wa Kimataifa na Maonesho ya Sayansi,Teknolojia na Ubunifu yaliyofanyika Juni 14 hadi 16 jijini Dar es Salaam.
Mario ambaye alikuwa mshindi wa kwanza katika Mashindano ya Kitaifa ya Ubunifu,Sayansi na Teknolojia (MAKISATU) kwa mwaka 2022 jijini Dodoma na kupata fursa ya kupewa zawadi na Makamu wa Rais Dkt.Philip Mpango na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema yeye binafsi na wenzake wamepata faraja kuona serikali inawathamini.
“Fedha hizo ingawa bado hatujakabidhiwa lakini si kazi rahisi kwa kuwa licha ya kuwa wabunifu lakini tulionesha tena ubunifu wetu katika maonesho hayo ambapo tulikuwa 20 na tuliobahatika kuchaguliwa ni saba hivyo tukajumuishwa na wenzetu wengine na tukafikia 49.
“Si unapewa fedha tu bali unachofanya lazima kionekane hivyo hata tukichukua fedha hizo lazima kuwe na nidhamu japokuwa si mkopo ili utakapoomba tena uweze kupewa.”amesema Mario
Awali akizungumza Machi 8,2023 mbele ya waandishi wa habari na watafiti jijini Dar es Salaam wakati wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kati ya waandishi wa habari na watafiti yaliyoandaliwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH),Mario amesema Tanzania inauwezo wa kuokoa dola za kimarekani Milioni sita za kuagiza Kaboni kutoka nje ya nchi.
Amesema Tanzania ni nchi ya 16 duniani kwa kuzalisha nazi baada ya nchi kama Indonesia,India,Brazil na Ufilipino hivyo kuna kiwango kikubwa cha nazi na ni fursa pia kwa watanzania kujua kuwa vifuu vya nazi ni mali inayoweza kuzalisha Kaboni.
“Baada ya kumaliza Chuo nilianza kufanya utafiti wa kuzalisha Kaboni na ndipo nilipobuni uzalishaji kwa kutumia vifuu vya nazi na baada ya kupimwa na kuthibitishwa imeonekana kuwa na uwezo wa asilimia 98 kukamata madini yaliyopo katika udongo”amesema Mario
Amesema kila mgodi wa dhababu lazima uwe na Kaboni kwa ajili ya kusaidia kukamatisha dhababu na Tanzania inahitaji tani 1500 pekee za Kaboni ambazo asilimia kubwa huingizwa kutoka nje ya nchi.




Discussion about this post