- NA GOODLUCK HONGO
WANYAMAPORI aina ya Tembo na Nyumbu wametajwa kuwa vinara wa kutumia ushoroba ambayo ni maeneo ya mapito ya wanyamapori kutoka eneo moja kwenda lingine kutafuta chakula na mahitaji mengine.
Mbali na kutafuta chakula lakini pia ni njia ambazo hutumiwa na wanyamapori wanapohama kutoka eneo moja kwenda eneo lingine kutafuta mahitaji yao yakiwemo madini ya chumvichumvi na kwenda kuzaliana kwa kubadilishana vinasaba na koo nyingine zilizopo mbali.
Hata hivyo mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira unaofanywa na binadamu umechangia wanyamapori kuhama kutoka eneo moja kwenda lingine kupitia njia hizo za asili.
Akizungumza na Bajeti Communication Juni 27,2023 jijiji Dar es Salaam kuhusu Shoroba,Kamishna Msaidizi kutoka Kanda ya Mashariki wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Keneth Sanga amesema ushoroba ni mapitio ya Wanyamapori ( Wildlife corridor) ambazo ni njia zinazotumiwa na wanyamapori kuhama kutoka eneo moja kwenda eneo lingine kutafuta mahitaji yao yakiwemo chakula, madini ya chumvichumvi pamoja na kuzaliana.
Amesema wanyamapori wanaotumia njia hizo mara nyingi wameonekana kuwa ni Tembo na Nyumbu ambao huzitumia kutoka Tanzania kwenda Kenya na Msumbuji.
“Wanyamapori wenye sifa za kutumia Shoroba hizi ni pamoja na Tembo na Nyumbu.
“Mfano wa Shoroba za Nyumbu ni Kaskazini mwa Tanzania ambapo nyumbu hutoka Hifadhi ya Taifa Serengeti na kwenda Hifadhi ya Maasai mara nchini Kenya.
“Ushoroba mwingine unapatikana Kusini mwa Tanzania ambapo Tembo hutoka Hifadhi ya Taifa ya Nyerere na Pori la Akiba Selous kuelekea nchini Msumbiji kwenye Hifadhi ya Niasa.”amesema Kamishna Msaidizi Sanga
Kamishna Msaidizi Sanga amebainisha kuwa licha ya changamoto za uvamizi wa Shoroba hizo lakini wameweka mikakati madhubuti ya kudhibiri uvamizi huo kwa kutumia mbinu mbalimbali ambazo ambazo ni pamoja na kufanya doria kwenye maeneo ya shoroba hizo mara kwa mara.
Aidha amezitaja mbinu zingine zinazotumika kulinda Shoroba hizo kuwa ni pamoja na kutoa elimu ya umuhimu wa shoroba kwa wananchi walio karibu na mapito hayo ya wanyamapori
“Njia nyingine ni kuwashirikisha wananchi katika uhifadhi wa shoroba mfano; Kuanzisha Hifadhi za Jamii (WMA) kama vile Mbarang’andu, Kimbanda, Kisungure, NALIKA na Chingoli zilizopo mkoani Ruvuma” amesema Kamishna Msaidizi Sanga
Hata hivyo uwepo wa shoroba hizo maarufu ndani na nje ya nchi zimechangiwa na juhudu kubwa za Serikali katika kuhakikisha kuwa shobora hizo hazivamiwi na binadamu kwa kuweka makazi ama mashamba ili kuwafanya wanyama hao kusafiri bila vikwazo katika eneo lao.
Awali akizungumzia na waandishi wa habari kutoka Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira (JET) kuhusu Shoroba,Meneja Ufuatiliaji na Tathmini Mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasili John Noronha amesema maisha ya wanyamapori na binadamu yanategemeana.
Amesema USAD kupitia mradi wake wa Tuhifadhi Maliasili ulianza Juni 2021 na unafanyakazi katika shoroba saba kati ya zaidi ya 60 zilizopo nchini na kutambuliwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (TAWA)
Baadhi ya Shoroba hizo ni pamoja na Kwakuchinja inayounganisha Tarangire na Manyara,Amani Dilu inayounganisha misitu ya hifadhi ya Amani iliyopo Muheza mkoani Tanga na Nyerere Selous Udzungwa mkoani Morogoro
Shoroba zingine ni pamoja na Ruaha Rungwa Katavi iliyopo kati ya Wilaya za Tanganyika na Uvinza mkoani Kigoma, inaoitwa Mahale Katavi inayounganisha Hifadhi ya Taifa ya Milima ya Mahale na Hifadhi ya Taifa ya Katavi.
Shoroba ya saba ambayo wanafanya kazi nayo ni ile ya Kigosi Moyowosi Burigi Chato inayounga mapori mawili ya Hifadhi ya Taifa ya Kigosi,mapori hayo ni Pori la Uwindaji la Moyowosi na Hifadhi ya Taifa ya Bugiri Chato iliyopo kari ya wilaya za Biharamulo mkoani Kagera na Kakongo mkoani Kigoma.
Hata hivyo ushirikishwaji wa viongozi na wananchi umetajwa kuwa ni muhimu katika kulinda mazingira na shoroba hizo kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.




Discussion about this post