NA GOODLUCK HONGO
AFISA Ufugaji Nyuki kutoka Idara ya Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii Aneth Moshi amesema Nyuki ni wadudu rafiki kwa mazingira hivyo wanatakiwa kutunzwa na kulindwa kutokana na umuhimu wake ikiwemo kuzalisha gundi.
Amesema baadhi ya tafiti zimeonesha kuwa Nyuki wanasaidia sana katika suala zima la uzalishaji wa chakula hivyo kukosekana kwao kutaongeza uhaba wa chakula.
Moshi ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaama wakati akizungumza na Bajeti Communication katika Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea katika viwanja vya Sabasaba.
Amesema mbali na mdudu huyo kuzalisha Asali,Nta na maziwa lakini pia huzalisha gundi ambayo hutumiwa katika kutengeneza dawa na vipodozi.
Amesema huwa hawapendi usumbufu kutoka kwa wadudu wengine ama madui zake hivyo hutumia gundi wanazozitoa katika miti mbalimbali na kuichukua na kisha kwenda kuziba eneo lao wanaloishi ili lisiingiliwe na wadudu wengine kama Mchwa,Sisimizi na Siafu.
Amesema Nyuki huchukua jukumu la kuweka gundi kwa ajili ya kuzuia maadaui muda wote ambapo hiyo ni moja ya njia ya kulinda kundi lao lisishambuliwe na maadui na ndipo huziba kila eneo na kuacha sehemu yao ya kuingilia pekee.
“Nyuki wanaweka gundi kwa ajili ya kuzuia maadui muda wote na hii ni moja wapo ya njia za kulinda kundi lao lisishambuliwe na maadui .
“Hawataki maadui kama siafu hivyo hutumia gundi kama ulinzi wake na hapo ndipo inapovunwa na baadaye kutengeneza dawa,vipodozi na hata chakula kutokana na mchanganyiko wa miti wanayotumia kutengeneza gundi hiyo”amesema Moshi
Hata hivyo Moshi amebainisha kuwa licha ya kuwepo kwa zao hilo la nyuki lakini bado wavunaji wake ni wachache.

Akizungumzia kuhusu mazao ya nyuki yanayotumika sana,Moshi ameeleza kuwa kwa sasa mazao ya Asali na Nta ndio yanayovunwa sana na mikoa inayoongoza kwa uvunaji huo ni Kanda ya Magharibi inayojumuisha Kigoma,Katavi na Tabora.
Kwa upande wa Kanda ya Ziwa ni Shinyanga ambayo huzalisha kidogo na Kanda ya Kati ni Dodoma na Singida ambapo Kanda ya Kaskazini ni pamoja na mikoa ya Arusha na Manyara huku Kanda ya Kusini ikiwakilishwa na Mtwara.
“Asali na Nta ndiyo yanayovunwa kwa wingi licha ya kuwa nyuki anazalisha maziwa na sumu yake ambavyo vyote ni muhimu lakini kutokana na changamoto mbalimbali Asali na Nta ndiyo yanaongoza kwa kuvunwa”amesema Moshi




Discussion about this post