NA MWANDISHI WETU
SERIKALI ya Tanzania inatumia kiasi cha Tsh. Bilioni 5.68 kuwalisha wahamiaji haramu wanaoikimbia machafuko katika nchi mbalimbali za Afrika na Asia.
Hata hivyo kuna wahamiaji haramu 4,419 walioko katika magereza mbalimbali nchini ambao wanatoka nchi mbalimbali, huku 1,264 wakiendelea kutumikia vifungo na wengine wakiwa wamemaliza lakini bado hawajaachiwa huru
Kwa mujibu wa Ripoti ya Mwaka ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles Kichere aliyoitoa Machi 29, 2023 kuhusu Ukaguzi wa Serikali Kuu kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Juni 30, 2022 ambapo amesema kuna wahamiaji haramu 3,110 magerezani ijapokuwa wamekamilisha adhabu za kifungo.
Amesema Kifungu cha 24 cha Sheria ya Uhamiaji (Sura ya 54) ya mwaka 2016 kinafanya kuwa ni kinyume cha sheria kwa wahamiaji haramu kuingia au kubaki Tanzania.
CAG Kichere amefafanua katika ripoti yake kuwa Kanuni namba 538 ya Kanuni za Kudumu za Magereza za mwaka 2003 inaeleza kuwa mtu anayesubiri kufukuzwa na kuwekwa kizuizini gerezani kwa mujibu wa masharti ya Sheria ya Wakimbizi ya mwaka 1998,anatakiwa kuchukuliwa kama mfungwa ambaye hajahukumiwa na kwa mujibu wa sheria na kanuni zote zinazotumika kwa tabaka hili la wafungwa.
“Katika ukaguzi wangu, nilibaini Idara ya Jeshi la Magereza ina wahamiaji 4,419 haramu kutoka nchi mbalimbali, huku 1,264 wakiendelea kutumikia vifungo, 45 wamewekwa mahabusu na 3,110 wanaotakiwa kurejeshwa makwao.
“Uwepo wa wafungwa ambao wamemaliza vifungo vyao lakini bado wako gerezani katika kipindi cha mwaka mmoja hadi mitano unatokana na kutokutolewa amri ya kuachiliwa huru na Wizara ya Mambo ya Ndani.
“Gharama za kuwahudumia wahamiaji hao ni kubwa, huku Chakula cha mfungwa mmoja kilitengewa bajeti ya Sh. 5,000 kwa siku, kitendo cha kuwa na wahamiaji 3,110 katika magereza hayo hugharimu Sh. Bilioni 5.68 kwa mwaka; hivyo kuipa mzigo serikali”amesema CAG Kichere
Hata hivyo CAG Kichere ameongeza kuwa Idara ya Jeshi la Magereza imeitaka Idara ya Uhamiaji kuchukua hatua stahiki za kuwarejesha makwao wahamiaji haramu wanaomaliza vifungo vyao ili kuepuka gharama za ziada.
“Waziri wa Mambo ya Ndani ametoa maagizo ya kuzuiliwa ili kuwabakisha wafungwa wa kigeni wanaohitaji kurejeshwa makwao,hata hivyo, kuwafukuza wahamiaji haramu ni suala la kidiplomasia linalohitaji mashauriano na Mabalozi wa nje ya nchi.
“Natoa wito kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, ikishirikiana na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kufanya juhudi zaidi kuhakikisha kwamba maagizo yanatolewa kikamilifu ili kuwarejesha raia wa kigeni walioachiliwa huru nchini kwao na kutatua suala hili kwa ukamilifu wake, na hivyo kupunguza gharama zisizo za lazima.”amebainisha CAG Kichere




Discussion about this post