NA MWANDISHI WETU,BUTIAMA
NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Jumanne Sagini na Mbunge wa Jimbo la Butiama ameshiriki Ibada ya mazishi ya marehemu Edward Magige ambaye ni Mjukuu wa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere, iliyofanyika kijijini kwao wilayani Butiama Mkoa wa Mara.
Marehemu Magige alifariki Novemba 11, 2023 kwa ajali iliyotokea huko mkoani Shinyanga,ambapo pia alikuwa mtumishi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ambacho ni moja kati ya chombo kilichopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi hadi umauti ulipomfika.
Huo unakuwa msiba wa pili ndani ya mwezi mmoja tangu kutokea kwa msiba wa kwanza wa marehemu Daudi Charles Makongoro ambaye ni mjukuu wa Baba wa Taifa na mtoto wa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Makongoro Nyerere aliyefariki Oktoba 29, 2023 kwa ajali ya gari iliyotokea katika barabara ya bypass Jijini Arusha.
Akizungumza katika mazishi hayo Novemba 14, 2023, Naibu Waziri Sagini ametoa pole kwa familia, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na Wafanyakazi wa NIDA Mkoa wa Shinyanga, ndugu, jamaa na marafiki na kuwaomba wazidi kumuombea marehemu aendelee kupumzika kwa amani.
“Baada ya kupata taarifa ya ajali pia nikaarifiwa kuwa alikuwa ni mtumishi wa NIDA huko mkoani Shinyanga na mimi kama Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi pia natoa pole kwa Mkurugenzi Mkuu na Watumishi wote,” amesema Sagini.
Aidha Viongozi mbalimbali wa Kiserikali, Kidini na Kisiasa walishiriki mazishi hayo akiwamo Mkuu wa Wilaya ya Butiama Moses Kaegele, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Mara Julius Masubo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Butiama ambaye pia ni baba mdogo wa marehemu Peter Wanzagi na Chifu wa Kabila la Wazanaki Japhet Wanzagi




Discussion about this post