NA MWANDISHI WETU,MARA
NAIBU Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Jumanne Sagini amefanya ziara ya kutembelea na kukagua Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara katika eneo la Manispaa ya Musoma unaogharimu zaidi ya Sh.Bilioni 1.4.
Akizungumza Novemba 16,2023 mkoani Mara muda mfupi baada ya kukagua ujenzi wa jengo hilo,Sagini amesema kukamilika kwa jengo hilo utaipa heshima na hadhi Ofisi ya Kamanda wa Polisi kwani kila Kitengo kitakuwa na Ofisi yake tofauti na ilivyo kuwa sasa.
“Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni sikivu na nimearifiwa kuwa, fedha za awamu ya pili na tatu tayari zimetoka hivyo basi nimuombe mkandarasi kukamilisha ujenzi kama inavyoelekeza ili ofisi ianze kutumika.” Alisema
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara ACP Salim Morcase, amemshukuru Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Wizara kwa ufuatiliaji wa karibu wa Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara.
“Sisi kama Jeshi la Polisi kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchi tunatoa shukrani zetu za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kwako kwa ufuatiliaji wa karibu wa Mradi wa Ujenzi wa Jengo letu”. amesema ACP Morcase

Aidha, amebainisha kuwa, Mradi huo mpaka sasa umefikia asilimia 92 na ulianza kutekelezwa Novemba 18, 2021 na unakadiriwa kumalizika mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka 2023.




Discussion about this post