LUANDA,ANGOLA
WATU 50 wamefariki dunia baada ya kunywa dawa ya mitishamba maarufu kama‘Mbulungo’ waliyopewa na waganga wa kienyeji ili kuthibitisha kama wao ni wachawi au sio.
Jeshi la Polisi nchini humo limethibitisha vifo vya watu hao baada ya kulazimishwa kunywa dawa hiyo ili kuthibitisha kwamba hawakuwa wachawi.
Kwa mujibu wa kituo cha RT kilichonukuu vyanzo vya taarifa hiyo,ilieleza kuwa vifo hivyo vilitokea katika kipindi cha miezi miwili iliyopita karibu na mji wa Camacupa, ambapo diwani wa eneo hilo Luzia Filemone alinukuliwa na redio ya taifa ya nchi hiyo kuwa waganga hao wa kienyeji walitumia mchanganyiko hatari katika taratibu hizo.
“Zaidi ya waathiriwa 50 walilazimishwa kunywa maji haya ya ajabu, ambayo yanathibitisha kama mtu anafanya uchawi au la,”amesema Filemone
Baadhi ya jamii za mashambani katika nchi hiyo ya Kusini mwa Afrika bado wana imani kubwa ya uchawi.
“Ni tabia iliyoenea sana kuwafanya watu wanywe sumu kwa sababu ya imani ya uchawi,” Msemaji wa Jeshi la Polisi Antonio Hossi amesema.
Hakuna sheria kuhusu vitendo vya uchawi nchini humo na iwapo watu wanashukiwa kuwa wachawi, wanalazimishwa kunywa mchanganyiko wa mitishamba wenye sumu unaojulikana kama ‘Mbulungo’.
Ikiwa watakufa kwa sababu hiyo, inachukuliwa kuwa ushahidi wa wao kuwa wachawi.




Discussion about this post