NA MWANDISHI WETU
WAZIRI wa Katiba na Sheria,Balozi, Dkt. Pindi Chana amesema uhusiano na ushirikiano baina ya nchi ya Tanzania na Urusi katika nyanja mbalimbali utazidi kuimarishwa kwa lengo la kuongeza tija na kuchochea maendeleo.
Hata hivyo Uhusiani kati ya Tanzania na Urusi ulianza tangu kipindi cha uongozi wa Hayati Mwl. Julius K. Nyerere.
Dkt. Chana ameyasema hayo Aprili 30,2024 mkoani Dar es Salaam alipokuwa akifungua rasmi mhadhara wa kitaaluma uliofanyika katika Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo (LST).
Akizungumzia umuhimu wa mhadhara huo, Balozi Dkt. Pindi Chana amesema kuwa wanafunzi wa sheria kwa vitendo walioshiriki katika mhadhara huo watapata faida kubwa kwa kulinganisha mambo mbalimbali ya kisheria kwa wenzao wa Urusi na kujifunza jinsi ya kutatua changamoto katika harakati za kujiweka salama, kisheria na kiuchumi.
Amesema kuwa tukio hilo ni fursa ya kudumisha na kutekeleza falsafa ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan inayojulikana kama 4R hivyo nchi lazima ishirikiane na nyingine ili kupata ujuzi na uzoefu kutoka kwa wageni.
Ameongeza kuwa mihadhara kama hiyo huleta tija kwa wanafunzi wa fani mbalimbali na kuwaongezea ufahamu na weledi katika masomo yao kwa manufaa yao na taifa.
“Urusi ni wazuri wa mambo ya Teknolojia katika ulinzi na usalama pamoja na masuala ya kisheria hivyo vijana wetu wakijifunza kutoka kwa wataalamu wataongeza ujuzi kwa manufaa yao na nchi yao” ameeleza Dkt. Pindi Chana.
Aidha, Dkt. Chana amesema wataalamu hao kutoka Ofisi ya Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Urusi wamekuja kutembelea Tanzania kwa shughuli za kujifunza na kudumisha uhusiano na ushirikiano uliokuwepo hata kabla ya Uhuru.

Kwa upande wake Balozi wa Shirikisho la Urusi nchini, Andrey Avetisyan ameeleza kufurahishwa na hatua kubwa za kimageuzi katika mifumo ya kisheria nchini Tanzania.
Aidha umefafanuwa kuwa anafurahishwa na mazingira rafiki na mazuri yanayowekwa na Serikali na Tanzania katika uwekezaji na biashara, huku akiwahimiza wawekezaji kutoka Urusi kuja kuwekeza Tanzania.

Naye Kaimu Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo (LST), Prof. Sist Mramba amesema kuwa kunahitajika ushirikiano wa kimataifa ili kukabili vitendo vya ugaidi na uhalifu wa kimtandao.
“Changamoto zinazoikabili dunia kwa sasa ni ugaidi na uhalifu wa mtandao hivyo kunahitajika ushirikiano wa mataifa mbalimbali katika kupeana ujuzi ili kukabiliana na changamoto zilizopo,” amesema Prof.Mramba.
Mhadhara huo umehudhuriwa na wanafunzi wa taasisi hiyo, wataalamu kutoka Urusi, wadau mbalimbali wa sheria pamoja na wahadhiri wa tasnia ya sheria kutoka vyuo vikuu hapa nchini.





Discussion about this post