NA GOODLUCK HONGO
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA) CPA Antony Kasore amesema mamlaka hiyo inatoa watu bora na wenye ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.
Mbali na soko la ajira lakini pia inatoa watu wenye ujuzi wa aina mbalimbali wanaohitajika na wawekezaji ikiwemo pia kujiajiri wenyewe.
Kauli ya CPA Kasore ameitoa Julai 6,2024 katika Banda la VETA wakati wa Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba yanayoendelea mkoani Dar es Salaam.
Amesema VETA hufanya utafiti wa soko la ajira kabla ya kuandaa mitaala ya kufundishia hivyo kurahisisha mahitaji ya wawekezaji wanaokuja kuwekeza nchini kupata watu wa kuwaajiri na kutoa fursa za ajira kwa watanzania.
‘’ Sisi VETA tunatoa watu wanaohitajika na wawekezaji,na huu ujuzi tunampatia mtanzania ataweza kuajiriwa sehemu mbalimbali ikiwemo Sekta ya Madini,Ujenzi, Utalii,Uchumi wa Buluu,Viwanda na maeneo mengine lakini pia anaweza kujiari mwenyewe na kujiingizia kipato.
‘’Sisi VETA tunaiangalia kauli mbiu ya Sabasaba inayosema “Tanzania ni Mahali Salama Pa Biashara na Uwekezaji” tunaiangalia katika kuhakikisha kuwa wawekezaji wanaokuja kuwekeza nchini wanapata watu wenye ujuzi wanaowahitaji katika fani zote’’amesema CPA Kasore
Hata hivyo CPA Kasore ameongeza kuwa VETA inatoa mafunzo hata kwa wahitimu wa Vyuo Vikuu na kwamba wakati mwingine hufika katika Vijiji na kuangalia fursa zilizopo katika eneo hilo na wao kuandaa mitaala yao ya kufundishia vijana kulingana na fursa zilizopo katika eneo hilo.
Kwa upande wake Mkufunzi wa Useremala wa VETA mkoani Tanga Yusuph Mkahallah amebainisha kuwa yeye anawafundisha vijana jinsi ya kutengeneza thamani za mbao ikiwemo sinia za mbao pamoja na ujasiriamali.
‘’Kwa upande wa ujasiriamali sisi tuna mashine ya kutotoleshea vifaranga vya kuku ambayo inauwezo wa kuweka trei 36 kwa wakati mmoja na ina uwezo wa kukaa masaa 36 bila kuwa na umeme.
‘’Sasa tukishamfundisha ujasiriamali kama huu pindi atakaporudi nyumbani basi ataweza kujiingizia kipato kwa utengenezaji wa thamani za mbao au kwa ujasiriamali huu wa kutumia mashine kutotolesha vifaranga vya kuku zaidi ya 10,000 kwa wakati mmoja’’amesema Mkahallah
Maonesho ya Sabasaba yenye Kauli Mbiu “Tanzania ni Mahali Salama Pa Biashara na Uwekezaji” yameanza Juni 28, 2024 na yanatarajiwa kufikia tamati Julai 14, 2024




Discussion about this post