NA GOODLUCK HONGO,LINDI
MAMLAKA ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA)imeanzisha mafunzo maalum kwa wafanyakazi wa nyumbani na kisha kuwatunuku vyeti baada ya kuhitimu.
Wafanyakazi hao wa majumbani wanafundishwa mambo mbalimbali ikiwemo kuwatunza na kuwapikia watoto,watu wazima na kufua kimataifa.
Akizungumza na Bajeti Communication mkoani Lindi Oktoba 30,2024 mara baada ya kutembelea chuo hicho,Mkuu wa Chuo cha VETA-Lindi Harry Mmari amesema pamoja na kutoa kozi mbalimbali za muda mfupi na mrefu lakini pia wameanzisha kozi ya maabara kwa mwaka 2025.
Amesema tayari maandalizi yote yamekamilika ikiwemo kuwasajili wanafunzi hao yanaendelea ambapo wakati chuo hicho kinaanzishwa walikuwa na wanafunzi 108 lakini kwa sasa wamefikia zaidi ya 400.
Amesema VETA huanzisha baadhi ya kozi kulingana na maeneo waliyopo ili kutoa fursa za ajira kwa vijana pindi wanapomaliza kwa kuwa na ujuzi.
‘’Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha kuwa chuo chetu kinafanikisha utoaji wa elimu ya ufundi kwa vijana kwa kutupatia fedha,lakini pia masomo tunayofundisha ni masomo ya kufanya kazi kwa vitendo.
‘’Ufundi stadi ndio unaoleta maendeleo katika nchi kwani hao ndio wanaujuzi wa kufanya kila kitu kama watu wenye fani mbalimbali ikiwemo umeme nyumbani na viwandani,ujenzi,ushonaji,udereva,ufundi bomba,magari na nk

Amesema kutokana na ongezeko la wanafunzi,tayari wameanza kuwa na changamoto ya mabweni kwani wana wanafunzi wa kutwa na bweni.
Akizungumzia kuhusu kozi wanayotoa ya wafanyakazi wa majumbani(house girl/boy) Mwalimu wa Mapishi,Huduma ya Vyakula na Vinywaji pamoja na Wafanyakazi wa majumbani wa chuo hicho Bernad Nkumba amesema wameamua kutoa kozi hiyo ili kuwaaidia wafanyakazi hao kufanya kazi zao kitaalamu.
Amesema hadi sasa VETA-Lindi imeshatoa wahitimu 80 wa kozi ya wafanyakazi wa majumbani na wote ni wanawake lakini pia hata wanaume wanakaribishwa kwa kuwa wapo na wanafanyakazi hizo bila utalaam.
‘’Tunawafundisha kuwapikia watoto wa rika mbalimbali wakiwemo wadogo na wakubwa kwa kuwa mtoto anavyokuwa na mazingira ya chakula chake yanabadilika,lakini pia tunawafundisha kuwapikia na kuwatunza wazee,wagonjwa na hata jinsi ya kutandika kitanda kimataifa.
‘’Tunawafundisha kufua kimataifa ikiwemo kutumia mashine ya kufulia kwa kuwa wengi wao huziona mashine hizi pindi wanapopata kazi lakini hapa anaijua mapema hivyo hatoshangaa atakapoiona.
‘’Mbali na hilo tunafundisha mapishi, kwa kuwa mchele sio mzuri kwa wazee kwani huwezi kumpa chakula chenye wanga nyingi mtu aliyezeeka hivyo kutokana na kuona hitaji hilo ndio sababu VETA-LINDI ikaamua kuanzisha kozi hiyo ambayo kwa sasa imekuwa na wanafunzi wengi’’amesema Nkunda

Nkunda amewaasa vijana wa kiume nchini kuachangamkia fursa hiyo kwa kuwa kwa kuwa ada yake ni nafuu.

Kwa upande wake Mwalimu Viyoyozi na Majokofu Kanda ya Kusini VETA-LINDI Frank Macha amesema wao wanawafundisha wanafunzi jinsi ya kutibu hewa.
‘’Kwa Kusini tumeona ongezeko la joto hivyo tunafundisha jinsi ya kufunga viyoyozi majumbani na tunawafundisha kazi ya jokofu ni kupooza lakini zingine zina sehemu ya kugandisha na kupooza.
‘’Tunawafundisha coldroom ambacho ni chumba maalum kinachotumika kuhifadhia miili ya watu waliofariki ambapo wanaweza kuhifadhiwa humo kwa muda mrefu hadi mwezi mzima.
‘’Majokofu ya kibiashara mengi huwa na vioo hivyo hutumika kupooza tu lakini coldroom hutumika pia viwandani hivyo wanafunzi wanapotoka hapa wanakuwa wataalam wa kutibu hewa’’amesema Macha
Macha amewaasa wazazi kuwapeleka watoto wao VETA ili waweze kupata ujuzi utakaowasaidia katika maisha yao.
Mbali na kozi hizo lakini pia VETA-Lindi inatoa mafunzo ya udereva wa mabasi,malori na magari madogo,jinsi ya kufunga CCTV Camera na fensi za umeme za majumbani na viwandani kwa kutumia mfumo maalum.



Discussion about this post