NA MWANDISHI WETU
MAMLAKA ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA) imepokea taarifa ya matokeo ya awali ya utafiti kuhusu matumizi ya makaa ya mawe na gesi asilia katika uzalishaji wa mbolea hususani zenye kirutubisho cha naitrojeni
Utafiti huo umefanywa na Kituo cha Kimataifa cha Maendeleo ya Mbolea (IFDC) chenye makao makuu yake nchini Marekani.
Akizungumza Novemba 12,2024 jijini Dar es Salaam mara baada ya hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Joel Laurent amesema, Serikali imepokea maoni yaliyotolewa na watafiti ya kufungamanisha Taasisi za Serikali katika uvunaji wa malighafi zinazopatikana nchini kwa manufaa mapana ya nchi.
Amesema, kufuatia utashi wa kisiasa uliopo, Serikali imeweka mazingira wezeshi ya kuhakikisha uwekezaji kwenye viwanda unawezekana kwa kutoa vivutio vya kikodi na visivyo vya kikodi pamoja na kuimarisha miundombinu ya usafirishaji kama barabara na reli na upatikanaji wa nishati ya kutosha.
Aidha, amesema TFRA itashirikiana na TPDC, GST na TIC ili kuwezesha matumizi ya malighafi zilizopo nchini katika uzalishaji wa mbolea na manufaa mengine kupitia wawekezaji watakaokuwa tayari kuwekeza.
Laurent ameongeza kuwa, kwa sasa kumekuwa na mwitikio mkubwa wa wakulima kutumia mbolea ambapo ndani ya miaka miwili,matumizi ya mbolea yameongezeka kutoka tani 360,000 hadi kufikia tani 840,000 na hivyo kutoa uhakika wa soko.
Amebainisha kuwa, uwepo wa malighafi za kuzalisha mbolea nchini ni fursa ya uwekezaji katika viwanda vya kuzalishaji mbolea ili kuhudumia soko la ndani na nchi zinazoizunguka Tanzania kutokana na nafasi nzuri ya kijiografia.
Mkurugenzi wa Idara ya Udhibiti kutoka TFRA, Elizabeth Bolle (mwenye suti nyeusi) akifuatilia taarifa ya utafiti wa uwekezaji kwenye viwanda vya mbolea kwa kutumia malighafi zinazopatikana nchini katika warsha iliyofanyika jijini Dar es Salaam Novemba 12,2024 jijini Dar es Salaam.

Akiwasilisha mada wakati wa warsha hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Mohamed Enterprises Tanzania Limited (MeTL) Indrabhuwan Singh amesema, Tanzania ina wigo mpana wa kuwekeza kwenye viwanda vya kuzalisha mbolea kutokana na uwepo wa viwanda vichache vinavyozalisha mbolea nchini.
‘‘Nchi yetu ina wazalishaji wachache wa mbolea ambao ni Yara, ITRACOM, Minjingu na wazalishaji wengine ambapo baadhi ya wazalishaji huchanganya mbolea kulingana na mahitaji ya udongo na mazao yanayolimwa.
‘’Huu ni wakati muafaka kwa wadau wa mbolea, Serikali, Taasisi za Fedha na wawekezaji kushirikiana ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuwa kapu la chakula (food basketi) kwa ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.
‘‘Sote tutajivunia kuona wakulima wakitumia mbolea zinazozalishwa hapa nchini,’’ameeleza Singh.
Kwa upande wake, Mshauri Elekezi wa IFDC kutoka ASNL Advisory Limited, Humphrey Simba amesema, utafiti uliofanyika unaonesha uwezo mkubwa wa nchi kujitosheleza kwa mbolea kutokana uwepo wa rasilimali zote muhimu za kuzalisha bidhaa hiyo ikiwa ni pamoja na makaa ya mawe, gesi asilia na umeme wa kutosha.
Simba ameleeza kuwa, IFDC kwa kushirikiana na USA Sera Bora Project wamefanya utafiti kwa kupita kwenye migodi ya makaa ya mawe iliyopo mkoani Ruvuma ili kujiridhisha na uwepo wa rasilimali hiyo ya kuzalisha mbolea.
“Lakini, pia tukapita kwenye miradi yetu ya gesi kule Mtwara na Songongo kuangalia kiwango cha makaa ya mawe, kuangalia kiwango cha gesi tulichonacho na namna ambavyo tunaweza tukatumia gesi na makaa ya mawe kwa ajili ya uzalishaji wa mbolea.” amebainisha Simba.
Simba amefafanuwa kuwa mkutano huo ulikuwa ni kwa ajili ya kufanya wasilisho la awali kwa yale ambayo yamebainika ambapo miongoni mwa mambo yaliyojitokeza ni uwepo wa makaa ya mawe na gesi ya kutosha na hivyo kuwezesha kuendelea kufanya majadiliano ya kina na Serikali ili kujua endapo vyote viwili vinaweza kutumika kwenye uzalishaji wa mbolea.
IFDC ni shirika lisilo la faida linalolenga Maendeleo Endelevu ya Kilimo na kuongeza usalama wa chakula duniani kwa kuongeza ufanisi wa matumizi ya mbolea, afya ya udongo, na uzalishaji wa mazao hasa katika nchi zinazoendelea.



Discussion about this post