NA GOODLUCK HONGO,DODOMA
SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limeendelea kuandika historia mpya baada ya Serikali kulipa kandarasi ya kujenga majengo ya Wizara nane katika Mji wa Serikali wa Mtumba jijini Dodoma.
NHC imejipatia sifa nzuri miongoni mwa Watanzania kutokana na ubunifu wake, utekelezaji, na usimamizi wa miradi ya ujenzi wa nyumba bora za makazi na biashara katika maeneo mbalimbali nchini.
NHC inayoongozwa na Mkurugenzi Mkuu wake Hamad Abdallah imekuwa ikijenga nyumba bora za kuuza na majengo ya biashara na kupangisha,lakini Shirika hilo ni moja ya wakandarasi bora waliopo nchini wanaojitosheleza kwa kila kitu.
Hata hivyo kutokana na uaminifu,kufuata viwango vya ujenzi kitaalam,kumaliza ujenzi kwa wakati ikiwemo kutumia vifaa bora vyenye viwango vinavyohitajika,Serikali iliamua kulipa kandarasi ya ujenzi wa majengo nane ya Wizara mbalimbali yakiwemo mawili wakiwa kama Washauri Elekezi Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) katika Mji wa Serikali Mtumba.

Akizungumzia juu ya NHC ni Mkandarasi Class A,Meneja wa Shirika hilo Mkoa wa Dodoma Gibson Mwaigomole anasema wanaishukuru Serikali kwa kuiamini Taasisi hiyo na hilo inaonesha kuwa Serikali ina imani kubwa sana na Shirika la Nyumba la Taifa kwa kuwapatia kazi kubwa katika Mji wa Serikali Mtumba.
‘’Sisi Shirika la Nyumba la Taifa ni Wakandarasi tena Wakandarasi Class A kabisa lakini pia ni Washauri Elekezi na katika eneo hili huko katika mikoa mingine tulishafanya katika maeneo tofauti tofauti lakini kwa Dodoma tulibahatika kupewa kazi kubwa na Serikali.
‘’Tunaishukuru sana Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha kuwa ina imani na Shirika letu kwani tumepewa kazi kubwa katika Mji wa Serikali Mtumba hapa Dodoma .
‘’Katika Mji huu sisi tunasimamia na kujenga Majengo ya Wizara nane ya Serikali lakini pia ni Washauri Elekezi katika Majengo ya Wizara mbili ambayo ni Jengo la Wizara ya Fedha lakini pia Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira.’’anasema Mwaigomole

Mwaigomole anaeleza kuwa katika majengo ambayo wanayajenga katika Mji wa Serikali Mtumba yaliyokaribia kumalizika yana thamani ya zaidi ya Sh.Bilioni 186 hivyo ni kazi kubwa lakini hadi sasa wameshafikia asilimia 88 hadi 90 ya ujenzi wa majengo hayo ambapo wapo katika hatua za mwisho katika kuyakamilisha.
Mwaigomole anayataja majengo ya Wizara hizo ambayo wanayasimamia na kuyajenga kama Mkandarasi Class A kuwa ni pamoja na Jengo la Wizara ya Mifugo,Jengo la Wizara ya Madini,Jengo la Wizara ya Viwanda na Biashara,Jengo la Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Jengo la Wizara ya Nishati,Jengo la Wizara ya Habari,Utamaduni Sanaa na Michezo,Jengo la Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Jengo la Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.
Mwaigomole anaongeza kuwa wana kazi kubwa katika Mkoa wa Dodoma hasa katika miradi ambayo wanaitekeleza kama wakandarasi lakini wanakwenda kuutua hivi karibuni kwa viwango bora na vya kisasa.
‘’Tunaishukuru Serikali kwa kutuamini na sisi tupenda tu kujiaminisha na kutoa ahadi ya ukweli kabisa kwamba tunakwenda kukamilisha hii miradi na hakutakuwa na tatizo lolote,quality iko vizuri,ni majengo ambayo ukiyaangalia unajua kabisa ni majengo yanayojengwa na Mkandarasi ambaye ni Taasisi zao ‘’anafafanuwa Mwaigomole

Kwa upande wake Mhandisi Ujenzi wa Shirika hilo anayesimamia majengo hayo katika Mji wa Serikali Mtumba Omary Chitawala anasema kwa ujumla kazi inaenda vizuri na wapo katika hatua za mwisho za kumalizia majengo hayo ambapo imefikia asilimia 90 ya ujenzi wake.
Anasema baadhi ya majengo kwa sasa yalipofikia wanamalizia kufunga baadhi ya vifaa ikiwemo taa,mifumo ya viyoyozi na mifumo ya kuashiria moto.
‘’Muda si mrefu tutakabidhi majengo haya,majengo haya yamezingatia sana ubora kwani vitu vyote ambavyo tumevitumia vimezingatia sana ubora wa hali ya juu lakini pia kuzingatia ushauri kutoka kwa Mshauri Elekezi.
‘’Ni majengo mazuri sana,kwa kweli na watumiaji wa majengo haya watakuja kufurahia sana kwa ubora wa majengo haya”anasema Mhandisi Chitawala

Akizungumzia kuhusu NHC ni Mkandarasi Class A,Mhandisi Chitawala anabainisha kuwa wao ni wakandarasi wakubwa na wanaojitosheleza kwa kila kitu ikiwemo vifaa,rasilimali watu pamoja na mambo yote yanayohusu ujenzi.

‘’Sisi tuko kamili na tumejitosheleza lakini pia sisi kama wakandarasi katika Mji huu wa Serikali Mtumba,tumeamiwa na Serikali na tumepewa majengo nane likiwemo la Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambalo mimi nasimamia na maendeleo ya miradi yote yanafanana na kwa mujibu wa mkataba tutaenda na muda ili tukabidhi”anaeleza Mhandisi Chitawala

Mhandisi Chitawala anaongeza kuwa baadhi ya majengo hayo yanajengwa kwa gharama ya zaidi ya Sh.Bilioni 22 kwa kila moja ambapo Jengo la Wizara ya Habari,Sanaa Utamaduni na Michezo linajengwa kwa Sh.Bilioni 22.8.
‘’Ujenzi ambao tumeufanya kwa majengo haya nane ,tunafurahi kwamba tumeufanya kwa viwango vya hali ya juu sana cha ubora,vitu vyote ambavyo tumetumia katika ujenzi wa majengo haya vimezingatia ubora ikiwemo nondo,kokoto na vingine vinavyotumika katika kuyamalizia majengo haya.
‘’Ukija na kuangalia kwa macho tu wewe mwenyewe utakubali tu kwamba hii kweli ni National Housing”anafafanuwa Mhandisi Chitawala





Discussion about this post