NA MWANDISHI WETU,MBEYA
WAZIRI wa Madini,Anthony Mavunde amesimamisha shughuli za uchimbaji madini zilizokuwa zikifanywa na Kampuni ya G & I Tech Mining Company Ltd kwa kipindi cha masika hadi itakapofanyika tathmini ya kitaalam ya mazingira juu ya shughuli za uchimbaji kwenye Mto Zila.
Mavunde ametoa agizo hilo Desemba 30, 2024 katika Kijiji cha Ifumbo, wilayani Chunya Mkoa wa Mbeya wakati alipotembelea eneo la leseni ya mwekezaji ambalo lilivamiwa na wananchi na kusababisha mgogoro mkubwa na uharibifu wa mali .
“Tumetembelea maeneo yote mawili, na sote tumejionea hali halisi ya mazingira,ni dhamira na maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuona shughuli zote za kiuchumi hususani za madini zinafanyika kwa utulivu bila kuleta migogoro na pasipo kuathiri mazingira ya eneo shughuli zinapofanyika.
‘’Nimesikiliza hoja za wananchi juu ya uharibifu wa mazingira ya Mto Zila,Serikali itaunda Timu ya wataalamu kufanya tathmini ya kina ya mazingira juu ya athari zinazoweza kutokea wakati wa uchimbaji wa madini na kwasasa shughuli zote za uchimbaji madini zisimame kipindi hiki cha masika kama Baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC ) ilivyoelekeza”amesema Mavunde

Amebainisha kuwa Wizara ya Madini kwa kushirikiana na watalaam wa mazingira, mkoa na wananchi katika muda mfupi ujao inakwenda kuunda Timu ya pamoja ya kufanya tathmini ili kueleza kitaalam iwapo shughuli hizo zinaweza kuendelea kufanyika pasipo athari kwenye mazingira ya Mto Zila.
‘’Nitumie fursa hii kuwataka wananchi wote kuacha vitendo vya uvunjifu wa amani na kujichukulia sheria mkononi,tunalaani kitendo cha kuvamia na kuharibu mali za mwekezaji“amesema Mavunde

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Juma Homera, amemshukuru Waziri Mavunde kwa kutembelea chunya na kuahidi kwamba atasimamia maelekezo yake ya kuona shughuli za uchimbaji katika Mto Zila zinasimama kipindi hiki cha masika mpaka pale watalaam watakapokamilisha taarifa ya tathmini na kutoa mapendekezo.
Awali, akitoa maelezo juu ya mgogoro huo, Mkuu wa Wilaya ya Chunya, Mbaraka Batenga amesema sasa anaona mwanga ambao unakwenda kuleta suluhisho la kudumu katika mgogoro baina ya mwekezaji na wananchi wa kijiji cha Ifumbo na kuwa Serikali ngazi ya wilaya itaendelea kusimamia sheria na kanuni ili kuhakikisha eneo hilo linakuwa salama muda wote.
Mbunge wa Jimbo la Chunya, Masache Kasaka kwa niaba ya wananchi ameishukuru Serikali kwa namna inavyoshughulikia changamoto za wananchi na kueleza kuwa ombi la wananchi ni kuona mazingira ya Mto Zila yanatunzwa kwa kuwa ni chanzo kikubwa cha maji kwa Wilaya ya Chunya.




Discussion about this post