NA GOODLUCK HONGO
TANI 28.7 na lita Milioni 5.4 za Kemikali Bashirifu ziliingizwa nchini mwaka 2023 pekee huku Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) ikizuia tani 159.3. na lita 1000 kutokana na ukiukwaji wa taratibu.
Kuzuiwa kwa tani hizo na DCEA ni muendelezo wa Taasisi hiyo ya Serikali katika kulinda afya za watanzania kupitia mapambano ya kutokomeza na kumaliza biashara ya dawa za kulevya nchini ambapo hadi sasa zaidi ya lita 19,804 za Kemikali Bashirifu tayari zimeshakamatwa.
Hata hivyo pamoja na mapambano na kazi kubwa inayofanywa na DCEA na vyombo vingine vya ulinzi na usalama lakini ‘’Mapapa wa biashara hiyo yameendelea kutumia mbinu mbalimbali ikiwemo ndege isiyo na rubani (drone) kufanikisha biashara yao hivyo kila mtanzania ana jukumu la kusaidia na kuhakikisha kuwa Taifa na kizazi chake kinakuwa salama dhidi ya ujangili wa biashara ya dawa kulevya na kemikali bashirifu.

Mwaka 2018 ndio mwaka unaoongoza kwa kuingizwa kwa tani nyingi za Kemikali Bashirifu ambayo ilifikia kiasi cha tani Milioni 1.5 ukifuatiwa na mwaka 2019 ulioingiza tani 249.8 huku mwaka 2017 ukiingiza tani 116.2,mwaka 2020 tani 96.0,2021 tani 3.65 huku mwaka 2022 ukiingiza tani 11.3.
Takwimu hizo zimetolewa na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) katika Taarifa ya Hali ya Dawa za Kulevya ya Mwaka 2023 iliyotolewa Mwezi Mei,2024.
Taarifa hiyo iliyosainiwa na Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo imeeleza kuwa DCEA hufuatilia taarifa mbalimbali za usafirishaji haramu wa Kemikali Bashirifu kupitia mifumo mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.
Kemikali Bashirifu huingizwa nchini kwa ajili ya shughuli za uzalishaji mali kwenye sekta mbalimbali kama vile bidhaa za viwandani,uchenjuaji madini katika migodi,kilimo,ujenzi,maji na katika kuboresha afya ya binadamu na mazingira.
‘’Kwa mujibu wa Taarifa za Msajili wa Kemikali nchini,kiasi cha tani 28.780.00 na lita za ujazo 5,432,147.35 za Kemikali Bashirifu ziliingizwa nchini kwa kipindi cha mwaka 2023.
‘’Kiasi cha tani 159.3 na lita 1000 za Kemikali Bashirifu zilizuiliwa kuingizwa kutokana na ukiukwaji wa taratibu’’
”Kemikali hizi zisipodhibitiwa zinaweza kuchepushwa na kutumika kutengeneza dawa za kulevya,kemikali hizo ni pamoja na Acetone,Toluene,Hydrochloric acid,Methylethylketone,Pseudoephedrine,Pottassium Permanganate na Ethyl ether’’imeeleza taarifa hiyo
Taarifa hiyo imeongeza kuwa mwaka 2017,DCEA ilizuia tani 250.1 za Kemikali Bashirifu kutokana na ukiukwaji wa taratibu ambapo mwaka 2018 ilizuia tani 23.1,2019 tani 43.6, 2020 tani 56.1,2021 tani 120.3, na mwaka 2022 ilizuia tani 98.3 la lita za ujazo 85.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo kwa upande wa lita za ujazo wa Kemikali Bashirifu zilizoingizwa nchini kuanzia mwaka 2017 imefafanuwa kuwa ni lita 13,016,446.00,2018 lita 11,247,555.00,2019 lita 6,304,971.00,2020 lita 4,256,161.00,2021 lita 855,807.00 na mwaka 2022 ni lita 5,711,266.00




Discussion about this post