NA ALEX KAZENGA
WALINZI wa Kampuni ya Ulinzi ya China Tanzania Security (CT) wanaolinda vituo vya Mabasi yaendayo Haraka (BRT) jijini Dar es Salaam, wamelalamikia hali ngumu ya maisha wanaopitia kutokana na kile walichoeleza kuwa hawajalipwa mshahara kwa zaidi ya miezi minne sasa.
Wakizungumza na Bajeti Communication mwishoni mwa wiki na kuomba kuhifadhiwa majina yao ili wasifukuzwe kazi kabla ya kulipwa haki zao,wamesema wamekuwa wakipokea ahadi ya kulipwa mishahara yao lakini ahadi hizo hazitekelezwi .
“Tunaishi maisha magumu mno, imefikia hatua kwa sababu ya kufanya kazi bila kulipwa baadhi ya wenzetu hasa wanawake wanalazimika kutumia njia zingine ambazo sio sahihi ili wapate namna ya kuishi.
“Walinzi wa kiume tunalazimika kufanyakazi nyingine za ziada kama kuendesha boda boda usiku, kulinda kwenye kumbi za starehe nyakazi za usiku ili tu tupate nauli na fedha nyingine za kujikimu tuwapo kwenye malindo ya CT,” amesema mmoja wa walinzi wa kampuni hiyo kwenye kituo cha mwendokasi Mbezi Luis.
Amesema pamoja na kufanyakazi bila mshahara lakini pia uongozi wa CT umekuwa hauzingatia haki zao za msingi kwa kuwakata fedha kwenye mishahara yao hasa wakichelewa kufika kazini kwa wakati.
Amefafanua kuwa kutokana na wao kufanyakazi bila kulipwa baadhi yao hukosa nauli ya kuwatoa nyumbani kwenda kwenye vituo vyao vya kazi, na kwamba anayefanikiwa kupata nauli na kwenda kazini kwa kuchelewa akifika tu huandikwa jina na kuelezwa kuwa siku CT itakayolipa mshahara atakatwa kiwango fulani cha fedha kwa sababu ya uchelewaji kazini.
“Wengi wetu tunashindwa kulalamika kwa sababu ukizungumza tu juu ya haki zako, uongozi wa CT haukusikilizi badala yake unaambiwa kama huwezi kazi uvue sare yao ya kazi na uondoke,” amebainisha mlinzi mwingine anayelinda kituo cha Mwendokasi Gerezani.
Akijibu tuhuma hizo,Mkuu wa Utawala na Sheria wa Kampuni ya CT, Paschal Temba, amekiri wazi kuwa hawajawalipa mishahara wafanyakazi hao kwa miezi minne huku akieleza kuwa hali hiyo imesababishwa na wao kuchelewa kulipwa na mteja wao ambaye ni DART.
“DART hawajatulipa kwa miezi 10 sasa, ndio maana hata sisi tunashindwa kuwalipa wafanyakazi wetu kwa wakati, wakisema kwamba tunawalaghai na kuwafanyia udanganyifu si kweli kwa sababu tumekuwa wawazi kwao.
“Kampuni haidanganyi wafanyakazi wake, tunatoa taarifa kwao lini tutawalipa kulingana na ahadi tunazopewa na DART, wakiona hatujawalipa mishahara yao ahadi tunayokuwa tumepewa inakuwa haijatimizwa na wateja wao,” anasema Temba.
Temba amefafanuwa kuwa ili kupambana na hali hiyo kampuni imekuwa na utaratibu wa kukopa fedha kutoka kwenye taasisi nyingine za kifedha na kulipa wafanyakazi wake huku ikizidi kusubiria kulipwa na mteja wake.
Hata hivyo Temba amepinga madai ya taasisi yao kunyanyasa wafanyakazi wake na kueleza kuwa haki zao zote zinazingatiwa na kwamba wanaohisi wanaonewa kwa kupatiwa adhabu ya kukatwa mishahara hasa kwa sababu ya uzembe kazini wanatakiwa kurejelea mikataba yao ya kazi inavyoeleza kabla ya kulalamika.
“Pamoja na hali mbaya ya kutolipana mishahara wapo wasichana hupita ofisini na kujieleza kuhusu hali zao na tunawapa advance salary.
“Kuna siku tunaona kabisa hali ni mbaya, ofisi inaamua kuwapa wafanyakazi wote Sh 10,000 na fedha hiyo hatuikati kwenye mshahara,” amebainisha Temba.
Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART0, Dk. Athuman Kihamia amebainisha kuwa malalamiko ya wafanyakazi wa kampuni ya CT hayaihusu DART na kwamba yeye si msemaji wa kampuni hiyo, hivyo haoni sababu ya kujibu chochote.
“Suala la wafanyakazi wa CT kutolipwa mishahara sisi DART tunahusikaje? Angalau mlalamikaji angekuwa ni uongozi wa CT hapo kungekuwa kuna hoja. Ikiwa anayelalamika ni mfanyakazi, hapo unataka nijibu nini? aulizwe mwajili wao,” amesema Dk.Kihamia




Discussion about this post