NA MWANDISHI WETU
MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imewatahadharisha Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni(Blogger), kuwa makini na taarifa zitakazochochea chuki na kuleta machafuko nchini hasa wakati huu kuelekea katika Uchaguzi Mkuu.
Mbali na hilo lakini pia TCRA imewahimiza Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni kuepuka kusambaza taarifa zitakazosababisha taharuki na ulipizaji wa kisasi ikiwemo kutopendelea upande wowote ili kuleta amani,umoja na mshikamano kwa jamii.
Kauli ya TCRA imekuja wakati ambapo watanzania wanatarajiwa kupiga kura ya kumchagua Rais,Wabunge na Madiwani katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025.
Akizungumza Agosti 3, 2025 mkoani Dar es Salaam wakati akiwasilisha mada katika mkutano ulioandaliwa na Tume Huru ya Uchaguzi nchini (INEC) kwa Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni, Meneja wa Huduma za Utangazaji kutoka TCRA,Mhandisi Andrew Kisaka amesema ni muhimu kwa Wazalidhaji hao wa Maudhui Mtandaoni kuepuka kuchapisha taarifa ambazo zitaleta taharuki na machafuko ndani ya nchi hasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.
Mhandisi Kisaka amebainisha kuwa wakati wa uchaguzi kuna mazingira ya migawanyiko, mivutano ya kijamii, na upotoshaji wa hali ya juu hivyo ni muhimu kwa Wazalishaji wa Maudhui Mtandaoni kuepuka kusambaza uvumi na kutangaza kwa umakini ikiwemo kutopendelea upande wowote na kukemea lugha za chuki.
Aidha amewataka wazalishaji hao nchini kote kuimarisha maadili yao na kuchukua jukumu muhimu katika kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani kwa kupandisha maudhui yenye tija na manufaa kwa Taifa.
“Kama unaona maudhui hayo yataleta taharuki ni bora kuachana nayo,vyombo vya habari vinaweza kujikuta vikichangia machafuko kwa kueneza uvumi au kuchochea upendeleo wa kisiasa kutokana na mazingira magumu na yenye shinikizo la juu la uchaguzi.”ameongeza Mhandisi Kisaka
Mhandisi Kisaka ametolea mfano wa machafuko ya uchaguzi yaliyotokea nchini Nigeria mwaka 2007 na Kenya 2011.
“Katika machafuko hayo zaidi ya watu 800 walipoteza uhai nchini Nigeria wakati nchini Kenya zaidi ya watu 1,000 walipoteza uhai na wengine 600,000 kupoteza makazi.
“Ili kukabiliana na maafa wakati wa uchaguzi na baada kuna miongozo ya utoaji wa taarifa ambayo inatatua changamoto hizo.
“Uvumi ndiyo chanzo kikuu cha vurugu hivyo Vyombo vya habari vinapaswa kuchunguza kwa umakini uvumi na kutoa taarifa sahihi na kwa haraka iwezekanavyo ili kuzuia mzunguko wa vurugu za kulipiza kisasi.” amesema Mhandisi Kisaka.
Hata hivyo Mhandisi Kisaka ameongeza kuwa vyombo vya habari havitakiwi kuchapisha taarifa ya kila kauli ya uchochezi kutoka kwa wanasiasa ,hata kama kauli hizo zinaonekana kuwa habari na zenye kuvutia msomaji ikiwemo lugha za kudhalilisha zinazoweza kuchochea wananchi kutenda vitendo vya kikatili.
Akizungumzia kuhusu urushaji wa matangazo mubashara kwa wazalishaji hao wa maudhui mtadaoni,Mhandisi Kisaka amefafanuwa kuwa katika kipindi hiki cha uchaguzi, ni muhimu wazalishaji hao kuchukua tahadhari binafsi ya kutoa matangazo mubashara(live) ya mikutano ya kampeni za wagombea kwa sababu yanaweza kuleta machafuko ikiwemo kuzuia kuonesha picha zinazochochea vurugeu na ikiwa ni lazima,basi pia kusimamisha matangazo hayo mubashara ili kuzuia hali kuwa mbaya zaidi.




Discussion about this post